Wednesday, September 30, 2015

ROCK CITY MARATHON 2015 YAZINDULIWA, KUTIMUA VUMBI NOVEMBA 15

 Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Dioniz Malinzi  (wa kwanza kushoto) akiwa kwenye hali ya furaha mara baada ya kuzindua msimu wa saba wa mbio za Rock City Marathon zinazotarajiwa kufanyika Novemba 15 mwaka huu katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza. Wengine ni pamoja na Meneja Mkuu wa kampuni ya Capital Plus International (CPI) ambao ndio warataibu wa mbio hizo Bw Erasto Kilawe (mwenye shati jeupe), Afisa Uhusiano Mwandamizi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) Bw. Salim Kimaro (wa pili kulia) na Bi Ummy Hassan kutoka idara ya Uhusiano NSSF ambao ni moja wa wadhamini wakuu wa mbio hizo.
 Meneja Mkuu wa kampuni ya Capital Plus International (CPI) warataibu wa mbio hizo Bw Erasto Kilawe (wa kwanza kushoto) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) wakati wa uzinduzi wa msimu wa saba wa mbio za Rock City Marathon zinazotarajiwa kufanyika Novemba 15 mwaka huu katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.  Wengine ni pamoja na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Dioniz Malinzi  (wa pili kushoto), Afisa Uhusiano Mwandamizi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) Bw. Salim Kimaro (wa tatu kushoto).

 Afisa Uhusiano Mwandamizi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) Bw. Salim Kimaro (wa pili kulia) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) wakati wa uzinduzi wa msimu wa saba wa mbio za Rock City Marathon zinazotarajiwa kufanyika Novemba 15 mwaka huu katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza. Wengine ni pamoja na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Dioniz Malinzi  (wa kwanza kushoto) na Bi Ummy Hassan kutoka idara ya Uhusiano NSSF ambao ni moja wa wadhamini wakuu wa mbio hizo.
Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Dioniz Malinzi  (wa tatu kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na waandaaji pamoja na wadhamini wa mbio za Rock City Marathon mara baada ya kuzindua rasmi msimu wa saba wa mbio hizo jijini Dar es Salaam jana. Mbio hizo zinazotarajiwa kufanyika Novemba 15 mwaka huu katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza. Wengine ni (kutoka kushoto) Katibu Mkuu wa BMT, Lihaya Henry,  Meneja Mkuu wa kampuni ya Capital Plus International (CPI) ambao ndio waratibu wa mbio hizo, Erasto Kilawe, Afisa Uhusiano Mwandamizi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) Bw. Salim Kimaro , Bi Ummy Hassan kutoka idara ya Uhusiano NSSF ambao ni moja wa wadhamini wakuu wa mbio hizo pamona na Katibu Mkuu msaidizi chama cha riadha Tanzania (RT) Bi. Ombeni  Savala .

Na Mwandishi Wetu.
Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Dioniz Malinzi, amezindua msimu wa saba wa mbio za Rock City Marathon zitakazofanyika Novemba 15 mwaka huu kwenye uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Mbio za Rock City Marathon, zinazoandaliwa na Kampuni ya Capital Plus International (CPI), kwa ushirikiano na Chama cha Riadha Tanzania (RT), pamoja na Chama cha Riadha Mkoa wa Mwanza (MRAA) zinalenga kutambua na kuinua vipaji vya wanariadha nchini na pia kukuza utalii wa ndani kupitia sekta ya michezo.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika jana jijini Dar es Salaam, Bw. Malinzi alisema baraza linafuraha kuona makampuni binafsi yakijiingiza katika kuinua mchezo wa riadha nchini.
“Mchezo wa riadha una changamoto kubwa na tunatambua jitihada zinazoendelea kufanywa na kampuni ya Capital Plus katika kurudisha hadhi ya mchezo  huu nchini kama ilivyokuwa miaka ya sabini na themanini,” alisema.
 Alisema kuwa Tanzania itarudi kileleni katika medani za michezo duniani kama wachezaji wataandaliwa katika viwango vinavyokubalika kimataifa.
“Inashangaza kuona taifa la watu milioni 45 linawakilishwa na wanariadha wachache sana, tena katika mbio ndefu huku tukikosa wanariadha wanaoliwakilisha vyema taifa katika mbio fupi,” alisema.
Akizungumza katika hafla hiyo, Meneja Mkuu kutoka kampuni ya Capital Plus International, Bw. Erasto Kilawe alisema kuwa mbio hizo zimekuwa zikionyesha mafanikio makubwa tangu kuanzishwa kwake mwaka 2009.
 “Jiji la Mwanza limebarikiwa kuwa na vivutio mbalimbali vya utalii. Jambo hili limetusukuma kuendelea kumulika vivutio vya kipekee vinavyopatikana katika ukanda wa ziwa Victoria kupitia mbio hizi,” alisema Bw. Kilawe huku akiongeza kuwa mikakati kabambe imewekwa ili kuhakikisha mbio za mwaka huu zinakuwa za mafanikio makubwa kuliko misimu iliyopita.
Alisema baadhi ya makampuni yameanza kujitokeza kudhamini mbio hizo ikiwa ni pamoja na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Precision Air, New Africa Hotel na Bank M huku makampuni zaidi yakionyesha nia ya kudhamini mbio hizo.
“Tunawaalika wadhamini waendelee kujitokeza kwa wingi ili kuzifanya mbio za mwaka huu kuwa bora zaidi,” alisema.
Uzinduzi huo ulihudhuriwa na wadau mbalimbali wa michezo ikiwa ni pamoja na wanariadha, viongozi wa vyama vya riadha, viongozi wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na wadau mbali mbali wa riadha nchini.
Kwa upande wake Afisa Uhusiano Mwandamizi wa NSSF , Salim Kimaro alisema kuwa shirika hilo limekuwa mstari wa mbele kudhamini mbio hizo kutokana ari yao katika kukuza hali ya michezo hapa nchini.
“Kwetu suala la michezo ni moja ya vipaumbele vyetu kutokana na ukweli kuwa michezo ni afya na pia ni sehemu ya ajira kwa vijana kwa sasa…tunaahidi kuwa mstari wa mbele katika kufaanikisha mbio hizi,’’ alisema.

No comments: