Friday, July 31, 2015

SHEREHE ZA NANE NANE KANDA YA KATI KUFANYIKA VIWANJA VYA NZUGUNI MKOANI DODOMA

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Chiku Gallawa akiwasilisha taarifa ya
maandalizi ya sherehe za Nane Nane Kanda ya Kati zitakazo fanyika
sambamba na Maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Kitaifa kuanzia Agosti
Mosi Mkoani Dodoma.

Sherehe za Nane Nane Kanda ya Kati zitafanyika sanjari na Maonesho na mashindano maalum ya mifugo ya 5 Kitaifa  katika  uwanja wa Nzuguni Dodoma kuanzia tarehe 01/08 hadi 08/08/2015.

Sherehe za Nane Nane mwaka huu 2015 zinakwenda kwa Kaulimbiu inayosema “Matokeo Makubwa sasa  (BRN)– Tuchague viongozi bora kwa maendeleo ya Kilimo na Ufugaji” Kaulimbiu hii imekuja wakati muafaka ambapo Taifa letu la Tanzania linaelekea katika Uchaguzi Mkuu Mwezi Oktoba na tayari baadhi ya vyama vya siasa vimeshaanza mchakato wa kuendesha kura za maoni ili kupata wagombea wa nafasi mbalimbali.

Kaulimbiu hii inatoa msisitizo kwa wananchi na watanzania wote kuchagua viongozi bora ambao watasaidia kuleta matokeo makubwa sasa katika nyanja za Kilimo na Ufugaji kwa maendeleo ya nchi yetu kwa ujumla.

Kama ilivyo ada,  Sherehe za Nane Nane Kanda ya Kati sanjari na Maonesho na mashindano maalum ya mifugo Kitaifa yanayofanyika kwenye viwanja vya Nzuguni hapa Dodoma, yameendelea  kuwa kitovu na chemchem ya elimu juu ya:  
  • Zana bora za Kilimo na Mifugo
  • Pembejeo za Kilimo na Mifugo
  • huduma za Mawasiliano ya Kibiashara
  • Usindikaji wa mazao ya kilimo na mifugo
  • taasisi mbalimbali za Fedha na Mabenki
  • Mafunzo na Utafiti na
  • taasisi za uzalishaji za Serikali.

Hadi kufikia sasa maandalizi muhimu kwa ajili ya kufanikisha Sherehe hizi za Nane Nane yapo katika hatua nzuri.

Maendeleo ya Vipando na Mabanda ya Mifugo kwa ujumla yapo katika hatua nzuri ingawaje hatua iliyofikiwa inatofautiana kati ya taasisi na taasisi.

Miundombinu ya Barabara Inapitika kirahisi, TASO kwa kushirikiana na Kamati ya Maandalizi ya Nane Nane Kanda ya Kati  inaendelea kufanya usafi wa barabara na kuhakikisha zinakuwa katika hali nzuri wakati wote wa Maonesho.

Huduma ya Maji inategemea mtandao wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dodoma (DUWASA) ambao ndiyo unaotumiwa na wadau wengi na visima virefu (9) ambavyo vimechimbwa  na wadau kwa matumizi yao. TASO Kanda ya Kati inaendelea kushughulikia changamoto ya kiufundi na kukatika kwa umeme kwa lengo la kuhakikisha maji hayakosekani kwenye viwanja vya Nane Nane Nzuguni.

Arena ya Mifugo imefanyiwa usafi na marekebisho madogo ili kuboresha mashindano maalum ya mifugo ya 5 Kitaifa. Kwa upande wa Mabanda ya Maonesho, Napenda kutoa wito kwa Wizara, Taasisi za Serikali, Taasisi zisizo za serikali , asasi na wadau mbalimbali kuendelea kukamilisha ujenzi wa mabanda yao ya maonesho kwenye viwanja vya Nzuguni ili kuleta ufanisi wa shughuli za Nane Nane.

Washindi wa Maonesho ya uwanjani: (Wakulima na Wafugaji bora) Kutakuwa na Majaji wasiopungua wanne (4) kutoka hapahapa Kanda ya Kati na  baadae washindi wa Maonesho watapewa zawadi kulingana na hali ya fedha, naomba nisitaje hapa  lakini niweke wazi kuwa Jukumu la kutoa zawadi ni la Kamati ya Maandalizi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Natumia fursa hii kuwakaribisha wakulima na wafugaji kutoka mikoa ya kanda ya kati na maeneo mengine ya Nchi, Wadau mbalimbali kuja kushiriki maonesho haya ya Nane Nane na pia nawakaribisha wananchi hususani wakulima, wafugaji, wasindikaji, wafanyabiashara na watoa huduma mbalimbali kuja kwa wingi kutembelea Maonesho ya Nane Nane na Maonesho na Mashindano maalumu ya mifugo kwenye viwanja vya Nzuguni Manispaa ya Dodoma kuanzia tarehe 1-8 Agosti, 2015 ili waweze kujifunza.

Kwa muhtasari matukio makuu kwa mujibu wa ratiba, katika siku ya ufunguzi na Kufunga Msisitizo utakua Kaulimbiu ya Maonesho, Siku ya Pili ya Maonesho Msisitizo utakua kuona Kiwango cha teknolojia ya Uzalishaji wa bidhaa za kilimo , mifugo, maliasili na viwanda katika kukuza uchumi.

Siku ya tatu ya Maonesho Msisitizo utakuwa Serikali za Mitaa kusimamia maendeleo vijijini; Siku ya nne msisitizo utakua juu ya sera ya mikopo kwa wakulima na wafugaji wadogo. Siku ya tano itahusisha Ufunguzi wa Maonesho na mashindano Maalumu ya tano (5) ya mifugo. Siku ya sita ya Maonesho msisitizo utakuwa kwenye umuhimu wa habari kwa maendeleo ya kilimo na mifugo. Siku ya saba msisitizo utakuwa kwenye Hifadhi ya Mazingira kwa kilimo na ufugaji endelevu.

Nawakaribisha sana wananchi na wadau mbalimbali wa kilimo na mifugo hapa Dodoma na Mikoa ya jirani kujitokeza kwa wingi kwenye Maonesho ya Mwaka huu, niweke mkazo kuwa ulinzi na usalama umewekwa vizuri ili kuhakikisha Maonesho hayo yanafanyika salama kwa utulivu na amani.

Katika hatua nyingine, kila Mwaka Tanzania huungana na nchi nyingine kuadhimisha ”Wiki ya Unyonyeshaji Maziwa ya Mama Duniani.” Maadhimisho haya yaliyoanza mwaka 1992, hufanyika kuanzia tarehe 01 – 07/08 ya kila mwaka.

Kwa mwaka huu 2015, Mkoa wa Dodoma Makao Makuu ya Nchi, umepewa heshima ya kuadhimisha Wiki ya Unyonyeshaji Maziwa ya Mama kitaifa. Maadhimisho haya yatakwenda sanjari na Sherehe za Nane Nane Kanda ya Kati na Maonesho na mashindano maalum ya mifugo ya 5 Kitaifa. Maadhimisho hayo yatafanyika kuanzia  Julai 1 - 7, 2015, ufunguzi utafanyika kwenye wilaya ya Chamwino kwenye Kijiji cha Nkwenda, wakati sherehe za Kilele cha Maadhimisho hayo Kitaifa zitafanyika hapa Manispaa ya Dodoma kwenye viwanja vya Maonesho ya Nane Nane Nzuguni.

Kaulimbiu ya Maadhimisho ya wiki ya unyonyeshaji maziwa ya mama  mwaka huu ni ”UNYONYESHAJI NA KAZI: TUHAKIKISHE INAWEZEKANA” (Breastfeeding and Work Lets Make it Work). Kaulimbiu hii inalenga kuwasaidia wanawake WOTE wanaofanya kazi katika sekta rasmi na isiyo rasmi waweze kutunza watoto wao ipasavyo pamoja na kufanya kazi mathalani kuajiriwa, kujiajiri, kazi za muda mfupi au mikataba na kazi zisizo za kulipwa kwa mfano kazi za mazingira ya nyumbani, shamba, mifugo na kutunza familia.

Katika maadhimisho ya mwaka huu, pamoja na masuala mengine muhimu, kutakuwa na utoaji wa elimu ya lishe kwa njia za vyombo vya habari, elimu ya lishe kwenye vituo vya kutolea huduma na eneo la Nane Nane, elimu ya lishe na unyonyeshaji kwa makundi ya wanafunzi, viongozi na Uhamasishaji kwa njia ya gari la maonesho na semina.

Hivyo natoa wito kwa wananchi wote wa Mkoa wa Dodoma na Mikoa ya jirani kuhudhuria ufunguzi na kilele cha maadhimisho haya ya Wiki ya Unyonyeshaji Maziwa ya Mama Kitaifa, halikadhalika, kutumia fursa hii adhimu kupata elimu juu ya masuala ya Unyonyeshaji na lishe ili kusaidia kumaliza tatizo la Utapiamlo baina ya wanawake walio katika umri wa kuzaa (15 – 49 yrs) halikadhalika kuondoa tatizo la utapiamlo kwa watoto wenye umri wa miezi 6 – 59.
                                             
Imetolewa na:
OFISI YA MKUU WA MKOA WA DODOMA
Julai 30, 2015.

No comments: