Sunday, December 30, 2012

Balozi Sefue ahimiza ushiriki wa Smart Partnership Dialogue


Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue (kulia) akijadiliana jambo kuhusiana na mkutano mkubwa wa kimataifa wa ushirikiano kwa manufaa ya wote, Smart Partnership Dialogue ‘Global 2013’, unaotarajiwa kufanyika hapa nchini mwezi Mei mwaka 2013 alipokua akiongea na wanahabari jijini la Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, (katikati) ni Kaimu katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC), Bw. Samson Chemponda na kushoto ni Meneja Mradi wa Smart Partnership Dialogue ‘Global 2013,’ Rosemary Jairo.
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue (kulia) akijadiliana jambo kuhusiana na mkutano mkubwa wa kimataifa wa ushirikiano kwa manufaa ya wote, Smart Partnership Dialogue ‘Global 2013’, unaotarajiwa kufanyika hapa nchini mwezi Mei mwaka 2013 alipokua akiongea na wanahabari jijini la Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, (katikati) ni Kaimu katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC), Bw. Samson Chemponda na kushoto ni Meneja Mradi wa Smart Partnership Dialogue ‘Global 2013,’ Rosemary Jairo.

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Viongozi katika ngazi mbalimbali Tanzania wamepewa changamoto kutoa umuhimu mkubwa na kushiriki kikamilifu katika majadiliano ya ushirikiano kwa manufaa ya wote (Smart Partnership Dialogue) ili kuchochea haraka maendeleo katika nchi.

Wito huu umetolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alipokua akiongea na waandishi wa habari kuhusiana na matayarisho ya mikutano ya kitaifa na ule wa kimataifa kuhusiana na majadiliano hayo hapa nchini.

“Ningewataka viongozi nao watoe umuhimu mkubwa kwenye jambo hili kwa sababu watanufaika sana kupata mawazo mbalimbali ya wananchi,” alisema Balozi Sefue mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa viongozi washiriki katika majadiliano katika ngazi zote kitaifa na pia wajiandae na majadiliano ya kimataifa.

Haya ni majadiliano yanayolenga kutoa fursa kwa jamii kukaa pamoja na kuzungumzia maswala mbalimbali ya maendeleo.

Kwa hapa Tanzania, chombo kitakachosimamia na kuratibu majadiliano haya kitaifa ni Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) wakati Wizara ya Mambo ya Nje ina jukumu la kuratibu mkutano wa kimataifa kuhusu majadiliano hayo hapa nchini mwezi Mei, 2013.

Mchakato wa majadiliano haya ulishazinduliwa na Rais Jakaya Kikwete tangu Mei, 2012.

Balozi Sefue ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Utendaji ya TNBC alisema kwamba kila mtanzania ajitahidi kuelewa dhana hii kwa kusoma na kusikiliza vyombo vya habari kwa sababu ni fursa nzuri kwa kila mwananchi kushiriki katika maendeleo ya nchi na namna tunavyoweza kufikia maendeleo ya haraka.

“Hakuna mwenye ukiritimba wa mawazo kwa hiyo tunahitaji mawazo ya kila mwananchi na hivyo kila mtu ajione kuwa ana wajibu wa kuchangia maana faida itakua kwa kila mmoja na nchi kwa ujumla,” alisema.

Alisema dhana hii ya majadiliano kwa manufaa ya wote ni muhimu sana hasa kwa viongozi kwa kuwa kadiri kiongozi anavyopata maoni ya watu wengi zaidi, ndio maamuzi yake yatakavyokua sahihi zaidi na yatazingatia mahitaji ya makundi mbalimbali katika jamii.

“Kwa mfano, maamuzi ya serikali yatakubalika kwa urahisi zaidi na wananchi kwa sababu watakua wameshiriki katika kuyaandaa,” alisema.

Akielezea zaidi alisema kujenga nchi kunahitaji makundi yote kwa hiyo ni vyema watu wakipata fursa nyingine kukakaa pamoja na kujadili mambo ya msingi ya maendeleo.

Alisema majadiliano kama haya ni fursa nyingine ya kushirikisha wananchi na wadau wengine katika kuhakikisha kuwa mipango katika kutekeleza Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 inazingatia maoni na inakua na faida kwa kila kundi katika jamii.

Mkutano wa mwezi Mei, 2013 ni mwendelezo wa mikutano kama hii ambayo imeanza kiasi cha miaka kumi na tano iliyopita na ikianzishwa na Jumuia ya Madola kupitia taasisi yake inayoitwa Commonwealth Partnership for Technology Management na kwa ushiriki mkubwa wa aliyekuwa waziri Mkuu wa Malaysia, Dkt. Mahathir Mohammed.

Tayari TNBC imeshaanza kuendesha semina za uhamasishaji zenye lengo la kutoa ufahamu kuhusu majadliliano ya kitaifa kabla ya yale ya kimataifa.

Kitaifa, majadiliano haya yatahusisha makundi mbalimbali yakihusisha serikali, wanasiasa, wafanyabiashara, wasomi,wafanyakazi, vijana, wasanii na wakulima ambao watakaa pamoja na kujadili maswala mbalimbali yanayohusu biashara na maendeleo.

Makundi haya yatapata fursa hiyo kupitia mabaraza ya mikoa na yale ya wilaya ya TNBC ambako madajiliano hayo yatafanyika kuanzia huko hadi ngazi za kitaifa kabla ya majadiliano ya kimataifa mwezi Mei.

Makundi yote yatapata fursa ya kujadili na kutoa mapendekezo yao.

No comments: