Tuesday, January 31, 2012

TUME YA VYUO VIKUU TANZANIA

(TANZANIA COMMISSION FOR UNIVERSITIES – TCU)

TAARIFA KWA UMMA KUHUSU UENDESHWAJI WA UDAHILI - ELIMU YA JUU KWA MWAKA WA MASOMO 2012/2013

UTANGULIZI

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (‘Tanzania Commission for Universities’-TCU) ikishirikiana na Baraza laTaifa la Elimu ya Ufundi (‘National Council for Technical Education’ - NACTE) pamoja na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi Elimu ya Juu (Higher Education Students Loans Board) inapenda kuutarifu umma kuhusu utaratibu wa kujiunga na vyuo vya elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2012/2013 kupitia mifumo ya “Pre-entry”, “Mature Age Entry”, “Equivalent Qualifications” na mfumo wa pamoja wa udahili (‘Central Admission System’) na utaratibu wa mikopo kama ifuatavyo:

MFUMO WA UDAHILI KUANZIA MWAKA 2012/13
1.1 Utaratibu wa Kuendesha Program za “Pre-entry” na “Mature Age Entry”

Kuanzia mwaka huu 2012, vyuo vyote vitakavyotaka kuendesha mafunzo ya awali kabla ya mwombaji kustahili kudahiliwa ili kuweza kujiunga na programu za elimu ya juu (pre-entry programmes) pamoja na kuendesha mitihani ya kupitia mfumo wa “Mature Age Entry” vinatakiwa kuwasilisha programu hizo Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) au Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) kwa uhakiki na kupata kibali. Programu hizo ni lazima ziendeshwe kwa muda wa mwaka mmoja. Hali kadhalika kwa upande wa mitihani kupitia mfumo wa mature entry, Tume kwa ushirikiano na Baraza, kwa pamoja wataandaa na kuratibu utaratibu wa mitihani katika vituo maalum kikanda ili vyeti vitakavyotolewa viwe na ulinganifu unaostahili na hatimaye kuweza kutumika katika udahili wa sifa linganishi katika vyuo mbalimbali.

Vyuo vinatakiwa kuandaa programu za mifumo ya “Pre-entry” na “Mature Age Entry” na kuziwasilisha Tume na Baraza ili zihakikiwe kwani mwaka wa masomo kwa kusudi hili utaanza mwezi Agosti 2012/2013. Kwa utaratibu huu, watakaofanya mafunzo hayo watatakiwa kufanya mitihani yao na kujiunga na masomo ya elimu ya juu katika mwaka wa masomo 2013/2014.

Kwa taarifa hii, mwaka 2012/13 hakutakuwapo na udahili wa wanafunzi kwa mfumo wa “Pre-Entry” na “Mature Age Entry”.

1.2 Utaratibu wa Udahili Kupitia Mfumo wa Pamoja (Central Admission System)

Waombaji watakaopitia mfumo wa pamoja wa udahili (CAS) wamegawanyika katika makundi manne, ambapo waombaji wa kundi (i), (ii) na (iii) watatambuliwa kama “Direct Applicants” na kundi (iv) watatambuliwa kama “Indirect Applicants”

Waliohitimu elimu ya sekondari kidato cha sita katika kipindi cha miaka miwili iliyopita pamoja na wale watakaohitimu mwaka huu.
Waliohitimu mafunzo ya diploma ya elimu ya ufundi (NTA level 6) kutoka vyuo vinavyotambulika na NACTE miaka miwili iliyopita pamoja na wale watakaohitimu mwaka huu;
Waliohitimu mafunzo ya Diploma ya Ualimu (kutoka vyuo vinavyotambulika) katika kipindi cha miaka miwili iliyopita pamoja na wale watakaohitimu mwaka huu.
Waombaji ambao sio wa moja kwa moja (Indirect Applicants) ni wote waliohitimu kidato cha sita, Diploma ya Elimu ya Ufundi (NTA level 6) na Diploma ya Ualimu katika kipindi cha zaidi ya miaka miwili iliyopita (kuanzia 2009 kurudi nyuma).
1.2 Waombaji Watakaowasilisha Maombi yao Moja kwa Moja Vyuoni

Waombaji watakaowasilisha maombi kupitia vyuo husika ni wenye sifa linganishi (Equivalent Qualifications) yaani wenye vyeti vya Astashahada na Diploma ambazo hazitambuliwi moja kwa moja na NACTE. Ili kukamilisha udahili, wanashauriwa kuwasiliana na NACTE ili vyeti vyao vitambuliwe na kusajiliwa kabla udahili haujaanza.

Vyuo vinavyofundisha programu mbalimbali katika ngazi ya Astashahada na Diploma ambavyo havina usajili wa NACTE/NECTA vinatakiwa kuwasilisha matokeo ya wanafunzi wao NACTE haraka iwezekanavyo ili matokeo hayo yaweze kutumika katika utambuzi wa vyeti vya wanafunzi husika.

MUDA WA UDAHILI KWA MAKUNDI MBALIMBALI
Muda wa maombi wa kuwasilisha maombi ya udahili kwenye CAS umegawanyika katika makundi matatu kama ifuatavyo:

Kundi la Kwanza – (1 Aprili mpaka 30 Aprili 2012)
Waombaji wote waliomaliza kidato cha sita, Diploma ya Elimu ya Ufundi (NTA level 6), na Diploma ya Ualimu kuanzia mwaka 2011 kurudi nyuma wataanza kuomba udahili kuanzia Aprili 1, 2012 hadi 30 Aprili 2012.

Kundi la Pili
Waombaji wote watakaomaliza kidato cha sita, Diploma ya Elimu ya Ufundi na Diploma ya Ualimu mwaka 2012 wataanza kuomba udahili baada ya matokeo yao ya mitihani kutangazwa na vyombo husika. Hakuna mwanafunzi atakayesajiliwa kwa kutumia matokeo ya muda (provisional or expected results).


Kundi la Tatu
Waombaji wote ambao ni raia wa Tanzania waliosoma nje ya nchi au wenye vyeti ambavyo si vya mfumo wa elimu ya Tanzania (mfano: Cambridge, Bacclaureate, n.k). Waombaji wa kundi hili wanashauriwa kuomba udahili mara matokeo yao yatakapotangazwa na watatakiwa kupeleka vyeti vyao Baraza la Taifa la Mitihani (“National Examinations Council of Tanzania – NECTA”) au Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (National Council for Technical Education - NACTE) kwa ajili ya kulinganisha alama zao za matokeo au kupata ithibati kabla ya kuanza kuomba udahili. Hakuna wanafunzi watakaodahiliwa kwa matokeo ya muda.

UTARATIBU WA MIKOPO
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu kwa mamlaka iliyopewa kisheria itatoa mwongozo na utaratibu wa utoaji wa mikopo mwezi Februari 2012. Miongozo hii itachapishwa katika vyombo vya habari na kusambazwa kwenye vyuo vyote vya elimu ya juu nchini na Ofisi za Posta na kwa Wakuu wa Elimu kila wilaya. Maombi ya mikopo kwa mwaka wa masomo 2011/2012 yataanza kupokelewa ifikapo mwezi Machi 2012 na mwisho wa kupokea maombi ni tarehe 30 Juni 2012. Utaratibu huu utahusu waombaji wote wapya na wale walioko masomoni katika vyuo vya elimu ya juu.

HITIMISHO
Tunapenda kuwajulisha waombaji wote kuzingatia muda wao wa udahili kama ulivyoainishwa katika tangazo hili. Muda ukiisha hawataweza kuomba hadi mwaka wa masomo 2013/2014. Pia waombaji wote wanashauriwa kufuata taratibu za mikopo kam zitakazotolewa na Bodi ya Mikopo ili kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza katika swala hili

Maelezo zaidi na ufafanuzi kuhusu udahili na mikopo wa 2012/13 yanapatikana katika tovuti zifuatazo:

Tume ya Vyuo Vikuu; www.tcu.go.tz

Baraza la taifa la elimu ya ufundi; www.nacte.go.tz

Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Elimu ya Juu; www.heslb.go.tz


IMETOLEWA NA: Katibu Mtendaji, Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania, S.L.B 6562, Dar es Salaam. Barua pepe (e-mail) es@tcu.go.tz

1 comment:

Anonymous said...

Ni mfumo mzuri kwani vyuo vingi vilikuwa vinatumia mfumo wa mature age entry kuwadahili wanafunzi wasio na sifa.Pia ni vizuri utaratibu huu ukavihusu hata vyuo vya private kwani vinadahili wanafunzi wasio na sifa kwa kutunga mitihani iliyo chini ya viwango ili kupata wateja wengi,wanafikiria zaidi maslahi ya kifedha na sio taaluma na hivyo baadaye kuleta usumbufu kwa serikali wanapokosa mikopo!